SIMULIZI ya mrembo mmoja ambaye jina lake halikupatikana mara
moja inatia majonzi na huzuni lakini habari mbaya zaidi ni kwamba
alifumaniwa na mwanaume wa mtu, katikati ya shamrashamra za Sikukuu ya
Wapendanao ‘Valentine’s Day’, akapewa kichapo hadi akazimia, Ijumaa
Wikienda linakupa zaidi.
Mrembo aliyefumaniwa akipatiwa huduma ya kwanza baada ya kuzimia.
Tukio hilo lililovuta hisia za watu wengi, lilitokea Februari 14, mwaka huu, katika ukumbi mmoja wa ‘kulia bata’ uliopo Temeke jijini Dar es Salaam.
HARUFU YA KASHESHE
Awali, paparazi wetu
aliyekuwa akijivinjari ukumbini humo akiwa na njaa ya habari, alimuona
dada huyo akiwa na mwanaume mmoja mtanashati wakiwa wamekaa chobingo
wakionekana kama vile ni mke na mume halali.
Wakiwa wamejiachia huku wakifurahia sikukuu hiyo ambayo kwa hapa Bongo imegeuzwa maana yake na kufanywa kuwa siku ya ngono, kamera ya Ijumaa Wikienda, iliamua kutulia kwa muda na kuwafuatilia.
Wawili hao walikuwa kivutio kikubwa miongoni mwa wapendanao
waliokuwemo ukumbini humo hasa kwa namna walivyovalia mavazi yao na
kupendeza.
Mrembo akiwa amezimia baada ya kipigo.
RANGI NYEKUNDU
Katika kile kilichoonekana mrembo
huyo alikuwa amepania sikukuu hiyo, alikuwa amevalia sketi na blauzi
nyekundu, zenye ‘material’ ya bazee na jamaa naye akiwa ametupia jinzi
la bluu na shati rangi ya damu ya mzee.
Wakiwa wanaendelea na stori za hapa na pale huku wakionekana kuwa
wamekolea kwa kinywaji, dada mmoja alipita eneo lile na kusimama kwa
muda mrefu akiwakazia macho, jambo lililomfanya paparazi wetu kuachana na mambo mengine na kusubiria kitakachotokea.
TIMBWILI
Haikuchukua hata dakika tano, yule dada
alirudi akiwa na kampani yake, huku mwanamke mmoja ambaye alijitaja
kuwa ni mke wa njemba yule akimvamia yule dada na kuanza kumpa kichapo.
“Nimekuvumilia sana wewe malaya, kwa nini unaniharibia maisha yangu?
Mume wangu hatulii nyumbani, mi nahangaika na watoto, wewe unakula raha
huku. Tena usivyo na haya umevaa na nguo mpya kabisa za Valentine, leo utanitambua,” dada huyo alisikika akisema kwa sauti huku akiendelea kumpa kichapo.
Jamaa (mume) alipoona soo limekuwa kubwa, alitimua mbio na kuacha timbwili likiendelea.
AZIMIA
Kipigo kilikuwa kikali na kwa bahati
mbaya watu walichelewa kuamulia ugomvi huo hali iliyosababisha mrembo
aliyekuwa akichezea kichapo kupoteza fahamu.
Wasamaria wema walipoona hali imekuwa mbaya kiasi kile, waliwaamulia,
kisha wakatoa taarifa kwa uongozi wa ukumbi ambapo viongozi walifika
haraka na kuwakamata mwanamke aliyekuwa akitoa kichapo na wapambe wake.
WAFUMANIAJI MIKONONI MWA POLISI
Wakati
walioanzisha vurumai lile wakiwa chini ya ulinzi huku mrembo yule
akipepewa, baunsa mmoja wa ukumbi huo alitoka nje na kuwaita polisi
ambao baada ya muda mfupi waliingia ukumbini humo.
Polisi hawakutaka kupoteza muda, waliwakamata wanawake hao kisha wakawatia pingu na kwenda nao kituoni.
Njiani, dada yule aliyekuwa amezimia alikuwa akiendelea kukupewa ili
aweze kupata hewa na kuzinduka, jambo ambalo halikuzaa matunda.
Habari zilipopatikana baadaye zilieleza kuwa, wanawake wale walitiwa
ndani baada ya kuchukuliwa maelezo yao wakati mrembo aliyechezea kichapo
akipelekwa katika Hospitali ya Mkoa wa Kitabibu, Temeke, Dar kwa
matibabu.
Zoezi hilo lilifanyika baada ya taarifa za mrembo huyo kuingizwa
kwenye fomu ya polisi nambari tatu ‘(PF3), huku waliompa kichapo
wakisubiri mrembo huyo apone ndipo shauri lao liendelee.
Hata hivyo, mrembo huyo alirejewa na fahamu muda mfupi baada ya kufikishwa hospitalini ambapo matibabu yalianza mara moja.