MKAZI wa Korogwe, mkoani Tanga ambaye inadaiwa alilazwa katika Hospitali ya Wagonjwa wa Akili Lutindi, wilayani humo,
hivi
karibuni alitoa kali ya mwaka baada ya kutoka wodini, kuingia katika
gari ambalo dereva wake alikuwa hajalizima na kuondoka nalo akiendesha
mwenyewe.
Tukio hilo lilivuta hisia za watu wengi
waishio jirani na hospitali hiyo, ambapo dereva wa gari hilo alifahamika
kwa jina moja la Bw. Wikama ambaye aliliacha gari hilo likiwa
halijazimwa.
Akizungumza na gazeti hili, Diwani wa Viti Maalumu
Tarafa ya Bungu, Bi. Elizabeth Singano, alisema mgonjwa huyo wa akili
ambaye jina lake halikuweza kupatikana mara moja, aliendesha
gari hilo na kushuka nalo katika milima yenye miteremko mikali
yenye kona bila wasiwasi wowote.
“Ilibidi
zipigwe simu ili kuomba msaaada wa kulizuia gari ndipo wananchi
waliamua kuweka magogo barabarani ili kulizuia,” alisema Bi. Singano
anayekaa kitongoji cha Bethelehemu
kilichopo jirani na hospitali hiyo.
Aliongeza
kuwa, Bw. Wikama alifika katika kituo hicho baada ya kupeleka mgonjwa
wa akili na alipoteremka kwenye gari hakulizima ndipo mgonjwa huyo
aliingia na kulichukua.
“Watu walishtuka walipoona mgonjwa wa
akili akiendesha gari, walianza kupiga kelele wakati akiondoka nalo
lakini mwenyewe hakuonesha waziwasi wowote,” alisema.
Majira
lilipomtafuta Bw. Wikama ambaye ni mkazi wa Donge, jijini humo kwa njia
ya simu ili kuzungumzia mkasa huo, alikiri kutokea tukio hilo na kudai
kuwa, asingependa kulizungumzia kwa kina kwani gari hilo ni mali ya
ofisi si la kwake.
“Ni kweli bwana mgonjwa wa akili aliendesha
gari nililokwenda nalo hospitali ila nisingependa kulizungumzia sana
tukio hilo, wapo watakaolipokea tofautina,” alisema Bw. Wikama ambaye
alipotakiwa kutaja namba za gari na aina yake alikata simu
na alipopigiwa tena hakupokea.
Hata
hivyo, Ofisa Utawala wa hospitali hiyo aliyefahamika kwa jina moja na
Bw. Lauth, alipoulizwa kuhusu tukio hilo alikiri kutokea kwa tukio hilo
na kudai mgonjwa huyo wamemrudisha Dar es Salaam.
Alisema tukio
hilo halikuwa la kawaida lakini limetokea kwa sababu aliyefika na gari
hospitalini hapo hakulizima kama ilivyo kawaida ya madereva wanaopeleka
wagonjwa ili kuepuka matukio ya aina hiyo.